
NAMNA YA KUFANYA UMRAH
Mtunzi
Sheikh Abdul-Aziz bin Abdillah bin Baaz
Sifa njema ni za Mwenyezi Mungu peke yake, na
baada ya hayo:
Huu ni muhtasari mfupi wa matendo ya ibada za
Umrah. Na kwa msomaji, maelezo ya hayo ndiyo
haya:
Mwenye kufanya Umrah atakapofika kwenye Miqat
(sehemu za kunuia Hija au Umrah), inapendekezwa
aoge na kujisafisha. Mwanamke pia atafanya hivyo
hata kama atakuwa katika hedhi au katika damu ya
baada ya kuzaa, isipokuwa hataruhusiwa kuzunguka
Ka'aba mpaka atwaharike na aoge.
Mwanamume anatakiwa kujipaka manukato kwenye
mwili wake kabla ya kuvaa nguo zake za ihram. Ikiwa
haitawezekana kuogea kwenye Miqat, basi hakuna
ubaya ikiwa ataoga anapofika Makka kabla ya
kuzunguka Ka'aba ikiwa hilo litawezekana.
Mwanamume atavua nguo zote za kawaida
zilizoshonwa na kuvaa kikoi na shuka, na
inapendekezwa ziwe nyeupe na safi.
Ama mwanamke, yeye atahirimia katika nguo za
kawaida (isipokuwa hatovaa nikabu, burka na glovu.
Hivyo atavivua na aufunike uso wake na mikono yake
kutokana na wanaume wasio mahram wake kwa nguo
nyinginezo) ambazo hazina mapambo wala si za
umaarufu.
2
Kisha ataweka nia ya kuingia katika ibada (ya Umra)
moyoni mwake na kuitamka kwa ulimi wake
akisema: “Labbayka umrah (Nimekuitikia kwa
kufanya Umra).” au “Allahummma labbayka umrah
(Ewe Mwenyezi Mungu, nimekuitikia kwa kufanya
Umra).”
Iwapo aliyehirimia Umrah atachelea kuwa
hatoweza kutekeleza ibada zake kwa sababu ni
mgonjwa au anaogopa adui au mfano wa hayo, basi
anaruhusiwa kuweka sharti anapohirimia kwa
kusema: "Ikiwa nitazuiliwa na kizuizi, basi mahali
pangu pa kutoka katika ihram ni pale
kitakaponizuilia." Haya ni kwa mujibu wa Hadithi ya
Dhwiba’ah bint Az-Zubayr, Mwenyezi Mungu
amuwiye radhi.
Kisha atafanya Talbiyah ya Mtume, rehema na
amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, ambayo
ni: Labbaika llaahumma labbaika. Labbaika laa
shariika laka labbaika. Innalhamda wanni'imata laka
walmulk laa shariika laka (NimekuitikIa ewe
Mwenyezi Mungu nimekuitikia! Nimekuitikia hauna
mshirika nimekuitikia. Hakika sifa njema na neema
na ufalme ni vyako, nimekuitikia huna mshirika!).
Anapoufikia Msikiti Mtakatifu, atautanguliza mguu
wake wa kulia wakati wa kuingia na aseme: "Kwa
jina la Mwenyezi Mungu, na rehema na amani ziwe
juu ya Mtume wa Mwenyezi Mungu. Ninajilinda kwa
Mwenyezi Mungu Mkuu, na kwa uso wake mtukufu,
na kwa utawala wake wa kale, kutokana na Shetani
aliyelaaniwa. Ewe Mwenyezi Mungu, nifungulie
milango ya rehema zako."
Anapofika kwenye Nyumba ambayo ni Ka’aba,
ataacha kufanya Talbiyah, kisha aende kwenye Jiwe
Jeusi, alielekee, kisha aliguse kwa mkono wake wa
kulia na kulibusu kama hilo litawezekana. Lakini
asiwaudhi watu kwa kuleta msongamano. Aseme
wakati anapoligusa: “Kwa jina la Mwenyezi Mungu,
na Mwenyezi Mungu ni Mkubwa." Kama itakuwa
vigumu kulibusu, ataligusa kwa mkono au kwa fimbo
au kwa kitu mfano wake, kisha akibusu kile
alicholigusa kwacho. Na kama itakuwa vigumu
kuligusa, basi ataliashiria na aseme: “Mwenyezi
Mungu ni Mkubwa.” na asibusu kile alichoashiria
kwacho.
Ili tawafu iwe sahihi, ni sharti kwamba mwenye
kutufu awe safi kutokana na hadathi ndogo na kubwa.
Kwa sababu, tawafu ni kama swala, isipokuwa
iliruhusiwa kuzungumza ndani yake.
Ataiweka Al-Ka’aba upande wake wa kushoto na
aizunguke mara saba. Kila anapofika kwenye kona ya
Yemeni, ataigusa kwa mkono wake wa kulia
4
ikiwezekana na kusema: “Kwa jina la Mwenyezi
Mungu, na Mwenyezi Mungu ni Mkubwa.” lakini
asiibusu. Ikiwa itakuwa vigumu kwake kuigusa,
ataiacha na kuendelea na tawafu yake, na asiiashirie
wala asiseme: "Mwenyezi Mungu ni mkubwa.” Kwa
sababu hilo halikusimuliwa kutoka kwa Mtume,
rehema na amani ziwe juu yake.
Ama Jiwe Jeusi, kila anapokuwa sawa nalo,
ataligusa na kulibusu kama tulivyotaja hapo awali.
Vinginevyo, ataliashiria tu na kusema: "Mwenyezi
Mungu ni Mkubwa." Inapendekezwa kutembea kwa
hatua za haraka fupi fupi katika mizunguko mitatu ya
kwanza ya Tawafu ya Kufika Makka, kwa wanaume
tu.
Pia inapendekezwa kwa mwanamume kufanya
Idhtwibaa katika Tawaf al-Qudum (Tawafu ya
kuingia Makka) katika mizunguko yote. Idhtwibaa
inamaanisha kuweka sehemu ya katikati ya upande
wa juu wa shuka yake chini ya kwapa lake la kulia na
ncha zake mbili kwenye bega lake la kushoto.
Na ni sunna pia kufanya dhikri na kuomba dua kwa
wingi, kiasi iwezekanavyo katika mizunguko yote.
Hakuna dua wala dhikri makhsusi katika tawafu.
Bali mtu ataomba na kumjata Mwenyezi Mungu kwa
dua na utajo wowote anaoweza. Na atasema baina ya
pembe mbili za Al-Ka'aba:
"Mola wetu Mlezi, tupe duniani mema, na Akhera
mema, na utulinde kutokana na adhabu ya Moto!"
Haya atayasema katika kila mzunguko. Kwa sababu,
hili lilithibiti kutoka kwa Mtume, rehema na amani za
Mwenyezi Mungu ziwe juu yake.
Ataumaliza mzunguko wa saba kwa kuligusa Jiwe
Jeusi na kulibusu ikiwezekana, au kuliashiria huku
akisema “Allahu Akbar (Mwenyezi Mungu ni
Mkubwa).” kulingana na maelezo yaliyotajwa kabla
ya muda mfupi. Baada ya kukamilisha mzunguko
huu, atavaa shuka lake kwa kuliweka juu ya mabega
yake na kona zake mbili za upande wa juu ataziweka
kwenye kifua chake.
Kisha ataswali rakaa mbili nyuma ya Maqam
Ibrahim ikiwa itakuwa rahisi kufanya hivyo. Lakini
kama hataweza kufanya hivyo, basi ataswalia mahali
popote pale Msikitini. Baada ya Al-Fatihah, atasoma:
“Sema, ‘Enyi makafiri.’ katika rakaa ya kwanza, na:
“Sema, ‘Yeye Mwenyezi Mungu ni wa Pekee.’”
katika rakaa ya pili. Hilo ndilo bora zaidi, lakini
akisoma kitu kingine, basi hakuna tatizo. Kisha,
baada ya kumaliza rakaa mbili hizi, ataelekea kwenye
Jiwe Jeusi, ikiwa hilo litawezekana.
Kisha atatoka aende kwenye Safaa na apande juu
yake au asimame hapo karibu. Kupanda juu yake
ndiyo bora zaidi ikiwezekana. Kisha atasoma maneno
ya Mwenyezi Mungu Mtukufu:
"Hakika vilima vya Safaa na Marwa ni katika alama
za Mwenyezi Mungu." [Al-Baqarah: 158]
Na inapendekezwa kwamba aelekee Kiblah, amsifu
na kumtukuza Mwenyezi Mungu. Atasema: “Hakuna
mungu ila Mwenyezi Mungu, na Mwenyezi Mungu
ni Mkubwa. Hakuna mungu isipokuwa Mwenyezi
Mungu asiye na mshirika. Ufalme ni wake, na sifa
njema ni zake, naye ni Muweza wa kila kitu. Hakuna
mungu ila Mwenyezi Mungu peke yake, alitekeleza
ahadi yake, na akamnusuru mja wake, na akayashinda
makundi (ya maadui) peke yake.” Kisha ataomba
awezacho huku ameinua juu mikono, na atairudia
dhikri hii na dua hii mara tatu.
Kisha atateremka na atembee akienda Marwah
mpaka afikie alama (taa ya rangi ya kijani kibichi), na
hapo mwanamume ataharakisha mwendo wa
kutembea mpaka afikie alama ya pili.
Ama mwanamke, yeye haruhusiwi kuharakisha
mwendo katika kutembea. Kwa sababu yeye ni uchi.
Kisha atatembea na kupanda juu ya Marwah au
kusimama hapo karibu. Kupanda juu yake ndiyo bora
zaidi ikiwezekana. Kisha atasema na kufanya juu ya
7
Marwah namna aliyoyasema na kuyafanya juu ya
Safaa. Kisha atateremka chini na kutembea katika
sehemu aliyotembea na kuongeza kasi katika sehemu
ambayo aliongeza kasi mpaka afike Safaa. Atafanya
hivyo mara saba. Kwenda kwake ni raundi, na kurudi
kwake ni raundi pia. Ikiwa atafanya sa'yi huku
amepanda, basi hakuna ubaya, hasa inapobidi.
Inapendekezwa kwamba afanye dhikri na kuomba
dua kwa wingi katika sa'yi yake awezavyo. Pia
inapendekezwa kwamba awe safi kutokana na
hadathi kubwa na ndogo. Hata hivyo, ikiwa ataifanya
bila twahara, basi hilo litamtosheleza.
Anapomaliza Sa’yi, mwanamume atanyoa nywele
za kichwa chake au atazifupisha. Kuzinyoa ndiyo
bora. Lakini ikiwa kuwasili kwake Makka ni karibu
na wakati wa Hija, basi kuzifupisha ndiyo bora kwake
ili aweze kunyoa sehemu ya kichwa chake iliyosalia
wakati wa Hija. Ama mwanamke, yeye atakusanya
nywele zake na kuzipunguza kiasi cha ncha ya kidole
au chini ya hivyo. Mtu aliyehirimia Umrah
atakapofanya kile kilichotajwa, basi Umrah yake
itakuwa imekamilika, na sifa njema ni za Mwenyezi
Mungu. Hapo, kila alichoharamishiwa kwa sababu ya
ihram, sasa kitakuwa halali kwake.
Mwenyezi Mungu atuwezeshe sisi na ndugu zetu
Waislamu wote katika kuifahamu dini yake na kuwa
imara ndani yake, na aikubali kutoka kwa kila mtu.
Kwani, Yeye aliyetakasika ni Mpaji, Mkarimu.
8
Na rehema na amani za Mwenyezi Mungu ziwe juu
ya mja wake na Mtume wake, Nabii wetu
Muhammad, na aali zake, Maswahaba wake, na
wafuasi wake waliomfuata kwa wema mpaka Siku ya
Malipo.
Mukhtasari Mfupi wa matendo ya ibada za Umrah.
Ulitolewa na Ofisi ya Mheshimiwa, mtunzi wake,
tarehe 13/2/1416 Hijria (Mkusanyiko wa Fatwa na
Makala ya Sheikh, Ibn Baaz 17/425 .
9