Nakala

Suala la usawa wa kijinsia ni muhimu, faafu, na linaloendana na wakati tulio nao. Mijadala na maandishi kuhusu mada hii inaongezeka na ipo katika mitazamo tofauti. Mtazamo wa Uislamu kuhusu suala hili umefahamika kwa uchache na kufasiriwa vibaya sana na wasio Waislamu na baadhi ya Waislamu vilevile. Makala hii imekusudiwa kutoa muhtasari na ufafanuzi sahihi wa msimamo wa Uislamu kuhusu suala hili.





Wanawake katika Tamaduni za Zamani


Ili uelewe vyema hadhi waliopewa wanawake kupitia Uislamu, mtu hana budi kuilinganisha na mifumo ya sheria nyingine zilizopo sasa na zilizokuwepo zamani.





(1)  Mfumo wa Uhindi: Imeelezwa katika Ensaiklopidia Britannica, ya 1911: “Huko India, kugandamizwa kulikuwa kanuni kuu.  Mchana na usiku wanawake sharti wawe chini ya walinzi wao katika hali ya utegemezi amesema Manu.  Sheria ya urithi iliegemea kuumeni zaidi, yaani wanaorithi wanafuatiliwa kutokana na nasaba ya kiume wakiwabagua wanawake.”  Katika maandiko ya Wahindu, wasifu wa mke mzuri ni kama ufuatao: “ni mwanamke ambaye mawazo yake, mazungumzo yake na mwili wake unaweza kudhibitiwa, ndiye hupata umashuhuri hapa duniani, na, kesho ahera, atapata makazi pamoja na mumewe.” (Mace, Ndoa ya Mashariki na Magharibi).





(2)  Mfumo wa Kigiriki: Huko Athene, wanawake hawakuwa tofauti sana na wale kutoka India wala Roma: “Wanawake wa Kiathenia daima walikuwa duni, wakiwa chini ya himaya ya baadhi ya wanaume - baba zao, kaka zao, au baadhi ya jamaa zao wa kiume.” (Allen, E. A., Historia ya Tamaduni).  Ridhaa yake katika ndoa haikuhitajika na “alilazimika atii matakwa ya wazazi wake, na kupokea kutoka kwao mumewe na bwana wake, hata kama ni mgeni kwake.” (Rejeleo Lililopita)





(3)  Mfumo wa Kirumi: Mwanamke wa Kirumi alisifiwa na mwanahistoria mmoja kuwa hivi: “mchanga, mdogo kiumri, anayelelewa, mtu asiyeweza kufanya kibinafsi au kwa niaba ya mwingine kitu chochote kwa kupenda kwake, mtu ambaye daima atakuwa chini ya usimamizi na ulezi wa mume wake.” (Rejeleo Lililopita).  Katika Ensaiklopidia Britannica, ya 1911, tunapata muhtasari wa hadhi ya kisheria ya wanawake katika utamaduni wa Warumi: “Katika Sheria ya Kirumi mwanamke alikuwa mtegemezi mno hata wakati wa matukio ya kihistoria.  Iwapo ameolewa, yeye na mali yake humilikiwa na mumewe . . . mke alikuwa bidhaa iliyonunuliwa na mumewe, mithili ya mtumwa aliyenunuliwa kutokana na manufaa yake.  Mwanamke hawezi kuchaguliwa au kushikilia wadhifa wowote wa kiserikali au wa umma . . . hawezi kuwa shahidi, mdhamini, mkufunzi, au mtunzaji; hawezi kupanga mtoto au kupangwa, au kuandika wasia au kufanya mkataba.”





(4)  Mfumo wa Kiskandinevia: Miongoni mwa koo za Waskandinevia wanawake walikuwa: “chini ya uangalizi wa kudumu, ikiwa wameolewa au hawajaolewa.  Katika enzi za baadaye za Kanuni za V za Wakristo, mwishoni mwa Karne ya 17, ilipitishwa kuwa iwapo mwanamke ataolewa bila idhini ya msimamizi wake, basi huyo msimamizi wake anaweza, akitaka, kusimamia na kuisarifu anavyopenda mali ya huyo mwanamke katika maisha yake yote.” (Katika Ensaiklopidia Britannica, ya 1911).





(5)  Mfumo wa Uingereza: Huko Uingereza, haki ya wanawake walioolewa ya kumiliki mali haikutambuliwa mpaka mwisho wa Karne ya 19, “Kupitia mfululizo wa sheria kuanzia Sheria ya Mali ya Wanawake Walioolewa ya 1870, iliyorekebishwa mnamo 1882 na 1887, wanawake walioolewa walifanikiwa kupata haki ya kumiliki mali na kuingia katika mikataba kama vile waseja, wajane, na watalaka.” (Ensaiklopidia Britannica, ya 1968).  Huko Ufaransa, hadi kufikia 1938, Sheria ya Ufaransa iliweza kurekebishwa ili kuwatambua wanawake kustahiki kufanya muamala wowote wa mkataba.  Mwanamke aliyeolewa, hata hivyo, bado alihitajika kupata idhini ya mumewe kabla hajaigawa au kutoa mali yake ya kibinafsi.





(6)  Katika Sheria za Musa (Kiyahudi): Mke alikuwa amechumbiwa.  Ikiieleza dhana hii, katika Ensaiklopidia Biblica, ya 1902, inafafanua: “Kumchumbia mke kunamaanisha kummiliki baada ya kulipa pesa; aliyechumbiwa ni msichana aliyelipiwa pesa.”  Kwa mtazamo wa kisheria, ridhaa ya mwanamke haikuhitajika kuhalalisha ndoa yake. “Ridhaa ya msichana sio muhimu na uhitaji wake haujapendekezwa popote katika Sheria.” (Rejeleo Lililopita).  Kuhusu haki ya talaka, tunasoma katika Ensaiklopidia Biblica: “Mwanamke akiwa mali ya mwanamume, kinachofuata ni kumpa mwanamume huyo haki ya kumtaliki kama jambo la kawaida.”  Haki ya kutaliki ilishikiliwa na mume tu, Katika Ensaiklopidia Britannica, 1911, inafafanua: “Katika Amri za Musa talaka ilimpendelea mume na kumpa yeye mahususi tu kuitekeleza...”





(7)  Kanisa la Kikristo: msimamo wa Kanisa la Kikristo hadi karne za hivi majuzi uliathirika sana na Amri za Musa pamoja na fikra zilizotiririka na kuenea katika mila za wakati huo.  Katika kitabu chao, Ndoa ya Mashariki na Magharibi, David na Vera Mace waliandika: “Mtu yeyote asidhaniye, halikadhalika, kwamba urithi wetu wa Kikristo hauwezi kuwa na mabezo ya hukumu.  Itakuwa shida sana kupata popote mkusanyiko wa marejeleo yanayomtweza mwanamke kuliko yaliyotolewa na Kanisa la akina Baba waasisi.  Lecky, mwanahistoria maarufu, anazungumzia juu ya ‘vichocheo hivi shadidi vinavyounda sehemu ya maandishi yaliyo bayana na ya kutisha ya akina Baba . . . mwanamke aliwakilishwa kama mlango wa jehanamu, kama chanzo cha maovu yote ya mwanadamu.  Anatakiwa aone aibu kuwa yeye ni mwanamke.  Anatakiwa aishi siku zote akitubia kutokana na laana aliyoiletea dunia.  Anatakiwa afedheheke na vazi lake, linalomkumbusha kuanguka kwake.  Anatakiwa afedheheke hasa na urembo wake, kwani ni silaha yenye nguvu ya shetani.’  Mojawapo wa mashambulizi makali dhidi ya mwanamke yanatoka kwa Tertullian: ‘Je, unajua kuwa kila mmoja wenu ni Hawa?  Hukumu ya Mungu kwa jinsia hii yenu inaishi katika zama hizi; lawama lazima ibaki leo pia.  Wewe ndiye mlango wa shetani; wewe ndiye mvunjaamri wa ule mti uliopigwa marufuku; wewe ndiye mhamaji wa kwanza wa sheria za Mungu; wewe ndiye nafsi ya kike aliyeshawishi nafsi ya kiume ambayo shetani hakuweza kuishambulia kirahisi.’ Sio tu Kanisa lilithibitisha hadhi duni ya mwanamke, pia lilimnyima haki zake za kisheria alizokuwa nazo hapo awali.”





Misingi ya Usawa wa Kiroho na Kiutu katika Uislamu


Katikati ya giza lililogubika dunia nzima katika Karne ya saba, wahyi kutoka kwa Mungu ulipiga mwangwi katika jangwa pana la Uarabuni kuleta ujumbe mpya, tukufu na kwa ajili ya walimwengu wote, unaoelezwa hapa chini.





(1)  Kulingana na Kurani Tukufu, wanaume na wanawake wana maumbile sawa ya kiroho:





“Enyi watu! Mcheni Mola wenu Mlezi, ambaye aliwaumba kutokana na nafsi moja na akamuumba kutokana na nafsi hiyo hiyo mwenza wake (mke wake) na akaeneza kutokana na wawili hao wanaume na wanawake wengi...” (Kurani 4:1, tazama pia 7:189, 42:11, 16:72, 32:9, na 15:29)





(2)  Mungu amewekeza katika jinsia zote mbili kwa heshima ya asili na amewapa madaraka wanaume na wanawake wote kuwa makhalifa au wadhamini wa Mungu ardhini (tazama Kurani 17:70 na 2:30).





(3)  Kurani haimlaumu mwanamke kuwa chanzo cha “kuporomoka kwa binadamu,” wala haichukulii ujauzito na kuzaa kuwa adhabu ya kuasi kwa “kula kutoka mti ulioharamishwa.”  Kinyume na hayo, Kurani inadhihirisha kuwa wote Adam na Hawa walifanya dhambi kwa pamoja ndani ya Bustani la Peponi, bila kumtenga Hawa ndiye wa kulaumiwa pekee.  Wote walitubia, na wakasamehewa kosa lao (tazama Kurani 2:36-37 na 7:19-27).  Kwa hakika, katika aya moja (Kurani 20:121) Adam alilaumiwa mahususi.  Kurani pia inathamini ujauzito na kuzaa kuwa miongoni mwa sababu tosha za akina mama kupendwa na kuheshimiwa na watoto wao (Kurani 31:14 na 46:15).





(4)  Wanaume na wanawake wana wajibu na majukumu sawa ya kidini na kimaadili.  Kila mwanadamu atalipwa malipo kulingana na amali au matendo yake:





“Na Mola wao akayakubali maombi yao (akajibu): Hakika sipotezi ujira wa kazi ya mfanyakazi (yeyote) miongoni mwenu, akiwa mwanamume au mwanamke, kwani ni nyinyi kwa nyinyi...” (Kurani 3:195, tazama pia 74:38, 16:97, 4:124, 33:35, na 57:12)





(5)  Kurani iko wazi kabisa kuhusu suala la madai ya ubora au udhalili wa mtu yeyote, awe mwanamume au mwanamke.  Linalozingatiwa katika msingi pekee wa ubora wa mtu yeyote juu ya mwingine ni uchaji Mungu na tabia njema, wala sio jinsia, rangi au utaifa (tazama Kurani 49:13).





Kipengee cha Uchumi wa Wanawake katika Uislamu


(1)  Haki ya Kumiliki Mali ya Kibinafsi: Uislamu umepitisha hukumu ya haki ya mwanamke aliyonyimwa kabla na baada ya Uislamu (hadi mwishomwisho wa karne hii), haki ya umiliki wa kibinafsi.  Sheria ya Kiislamu inatambua haki kamili za mali kabla na baada ya ndoa.  Wao wanaweza kununua, kuuza, au kukodisha mojawapo wa au zote za mali zao wanavyopenda.  Kwa sababu hii, wanawake wa Kiislamu wanaweza kuendelea kuitwa (na bila shaka yoyote wamekuwa kwa kawaida wakiitwa) kwa majina yao ya utotoni baada ya kuolewa, kama ishara ya uhuru wao wa haki ya kumiliki kisheria.





(2)  Usalama wa Kifedha na Sheria za Mirathi: Usalama wa kifedha umehakikishiwa wanawake.  Wana haki kupokea zawadi za ndoa au mahari bila kikomo na kuendelea kumiliki mali zao na mapato yao wakati wa sasa na wa baadaye kwa ajili ya usalama wao, hata baada ya ndoa.  Hakuna mwanamke yeyote aliyeolewa anahitajika kutumia kiasi chochote kutoka kwa mali zake au mapato yake kwa ajili ya matumizi ya nyumbani.  Mwanamke pia ana haki ya kupewa masurufu yake kamili wakati wa ndoa na wakati wa 'kipindi cha kusubiri' (eda) ikiwa ameachwa au amefiliwa.  Wanazuoni wengine wanalazimisha, kuongezwa, msaada wa mwaka mmoja kupewa mtalaka na mjane (au aliyeachwa mpaka warejeleane, iwapo kurudiana kuoana kutatokea kabla ya mwaka kwisha).  Mwanamke anayebeba au kujifungua mtoto ndani ya ndoa ana haki ya kupewa masurufu ya mtoto na baba mzazi.  Kwa ujumla, mwanamke wa Kiislamu anahakikishiwa kupewa msaada wa kifedha katika hatua zake zote za maisha, kama binti, mke, mama, au dada.  Ingawa wanawake, na sio wanaume, wamepewa kipaumbele katika matumizi ya kifedha katika ndoa na familia, Kurani vilevile imempa mwanamume mafungu mara mbili kuliko mwanamke katika sheria ya mirathi ili kusawazisha hayo.  Wanaume hawarithi zaidi kila wakati; mara nyingine mwanamke hurithi zaidi ya mwanamume. Endapo wanaume watarithi zaidi bado watawajibika kifedha kuwaangalia jamaa zao wa kike: wake, mabinti, mama, na dada zao.  Wanawake hurithi kidogo lakini wataendelea kuhifadhi mgao wao wa uwekezaji na usalama wa kifedha, bila ya kuwajibika kisheria kutumia sehemu yao yoyote ile, hata kwa kujikimu wenyewe (kwa ajili ya chakula, mavazi, malazi, matibabu, n.k.).  Ikumbukwe kuwa kabla ya Uislamu, wanawake wenyewe walikuwa wakirithiwa pia (tazama Kurani 4:19).  Katika baadhi ya nchi za kimagharibi, hata baada ya kuja kwa Uislamu, urathi wote wa marehemu ulipewa mtoto mkubwa (wa kwanza) wa kiume.  Hata hivyo, Kurani iliweka wazi kuwa wote wanaume na wanawake wana haki kupata mgao maalumu wa urathi wa wazazi wao waliokufa au jamaa zao wa karibu.  Mungu anasema:





“Wanaume wanayo sehemu katika walichokiacha wazazi na jamaa wa karibu, na wanawake wanayo sehemu katika walichokiacha wazazi na jamaa wa karibu, kiwe kidogo au kingi, mgao uliofaridhiwa.” (Kurani 4:7)





(3)  Ajira: Kuhusu haki ya mwanamke kutafuta kazi, ni sharti ibainike kwanza kuwa Uislamu unazingatia nafasi yake katika jamii kama mama na mke kuwa adhimu na muhimu zaidi.  Hakuna wajakazi wala mlezi wa watotot wa muda wanaoweza kuchukua nafasi ya mama kama mwalimu wa mwana aliyenyooka, asiye na hisia za kujitwaza au kujitweza, na aliyeleleka kwa misingi imara.  Hilo ni jukumu bora na muhimu, ambalo kwa kiasi kikubwa linaunda mustakabali wa mataifa, haliwezi kamwe kuzingatiwa kama uvivu.  Walakini, hakuna amri katika Uislamu ambayo inakataza wanawake kutafuta ajira wakati wowote kunapotokea haja ya kufanya hivyo, hasa katika nafasi ambazo zinachukuana barabara na maumbile yake, na ambayo jamii inamuhitajia zaidi.  Mifano ya kazi hizo za kitaaluma ni uuguzi, ualimu (kufunza hasa watoto), utabibu, na kazi za kijamii na za kutoa misaada.





Kipengee cha Kijamii cha Wanawake katika Uislamu


A)        Kama Binti:


(1)  Kurani ilimaliza ada ya uuaji katili wa mtoto mchanga wa kike, iliyotendeka kabla ya Uislamu. Mwenyezi Mungu anasema:





“Na msichana aliyezikwa hai atakapoulizwa, kwa kosa gani aliuliwa?” (Kurani 81:8-9)





(2)  Kurani iliendelea kukemea tabia isiyokubalika ya baadhi ya wazazi wanaposikia taarifa ya kuzaliwa kwa mtoto wa kike, badala ya mtoto wa kiume. Mungu anasema:





“Na mmoja wao akibashiriwa (kuzaliwa) kwa msichana, uso wake unasawijika, naye anajaa chuki. Anajificha asionekane na watu kutokana na habari mbaya aliyojulishwa; Je, akae naye juu ya fedheha hiyo au amfukie udongoni? Tazama uovu wa wanavyohukumu.” (Kurani 16:58-59)





(3)  Wazazi wanawajibika kuwasaidia na kuwaonyesha huruma na uadilifu kwa mabinti zao. Mtume Muhammad, rehema na amani zimshukie, alisema: “Yeyote atakayewalea mabinti wawili mpaka wakomae (umri wa kupevuka), yeye na mimi tutakuwa pamoja Siku ya Kiyama kama hivi (na akaashiria kwa vidole vyake vikishikana)."





(4)  Elimu ni kipengee muhimu katika malezi ya mabinti ambayo huathiri sana maisha yao ya baadaye.  Elimu sio tu ni haki bali ni jukumu la wanaume na wanawake wote. Mtume Muhammad alisema: "Kutafuta elimu ni lazima kwa kila Muislamu." Neno "Muislamu" hapa linahusisha wanaume na wanawake.





(5)  Uislamu hauhitaji wala hauhimizi kupasha tohara wanawake. Ingawa kuna Waislamu wengine kutoka sehemu fulani za bara la Afrika hutekeleza hilo, pamoja na Wakristo katika maeneo hayo, hilo lichukuliwe tu kuwa kama mila na desturi za huko.





B)        Kama Mke:


(1)  Ndoa katika Uislamu imejengwa katika msingi wa amani kutoka pande zote, upendo, na huruma, na sio tu kutosheleza hamu na uchu wa kibinadamu. Miongoni mwa aya zinazovutia sana katika Kurani kuhusu ndoa ni ifuatayo:





        “Na katika ishara zake ni: kuwa amekuumbieni wake zenu kutokana na nafsi zenu ili mpate utulivu kwao; naye amejaalia mapenzi na huruma baina yenu. Hakika katika haya zipo ishara kwa watu wanaofikiri.” (Kurani 30:21, tazama pia 42:11 na 2:228)





(2)  Mwanamke ana haki ya kukubali au kukataa posa ya ndoa. Kulingana na Sheria ya Kiislamu, wanawake hawafai kulazimishwa kuolewa na mtu yoyote bila idhini yao.





(3)  Mume ana majukumu ya kukimu haja zake , kumlinda, na kutoa uongozi wa jumla kwa familia, katika mfumo wa mashauriano (tazama Quran 2: 233) na huruma (tazama Quran 4:19). Hali ya mapatano  na kukamilisha  kwa majukumu ya mume na mke haimaanishi utiifu  kutoka upande mmoja kwa upande mwingine. Mtume Muhammad aliwaamrisha Waislamu kuhusu wanawake: “Ninakuhimiza uwe mzuri kwa wanawake.” Na "Walio bora kati yenu ni wale ambao ni bora kwa wake zao." Kitabu kitakatifu cha Qur'ani kinasihi  waume kuwa wema na kuwajali wake zao, hata kama mke atakosa fadhila za mumewe ama ukosefu wa ari kuibuka ndani yake:





“...Na kaeni nao kwa wema, na ikiwa  mmewachukia, basi huenda mkakichukia kitu, na Mwenyezi Mungu ametia kheri nyingi ndani yake.” (Kurani 4:19)





Pia iliharamisha desturi za Kiarabu kabla ya kuenea kwa Uislamu ambazo mtoto wa kambo wa baba aliyekufa aliruhusiwa kumiliki mjane (wajane) wa baba yake (kuwarithi) kana kwamba walikuwa sehemu ya mali ya marehemu (tazama Kurani 4:19).





(4)  Pindi mizozo ya ndoa ikitokea, kitabu kitakatifu cha Kurani kinahimiza wachumba kutatua matatizo yao faraghani kwa haki na wema. Kwa kweli, kitabu kitakatifu cha Kurani kinaelezea hatua ya kuelimisha kwa njia ya busara kwa mume na mke ya kutatua mizozo inayoendelea katika maisha yao ya ndoa. Iwapo itajulikana kwamba mzozo hauwezi kusuluhishwa kwa usawa kati ya mume na mke, kitabu kitakatifu cha Kurani inashauri kuingilia kati kwa familia ili kuleta suluhu kwa wahusika kwa niaba ya wachumba wote wawili (tazama Kurani 4:35).





(5)  Talaka ni njia ya mwisho, inakubalika lakini haihimizwi, kwani kitabu kitakatifu cha Kurani kinaenzi uhifadhi wa imani na haki ya mtu-wa kiume na wa kike kwa ufasaha. Njia za kuvunjika kwa ndoa ni pamoja na makubaliano ya pande zote, ari ya mume na mke (ikiwa ni sehemu ya mkataba wake wa ndoa), uamuzi wa korti juu ya ari ya mke (kwa sababu halali), na ari ya mke bila sababu ya msingi, basi mwanamke atalazimika kurejesha mahari kwa mumewe. Iwapo mwendelezo wa uhusiano wa ndoa hauwezekani kwa sababu yoyote, wanaume bado wanafundishwa kuvunja ndoa kwa njia nzuri. Kitabu kitakatifu cha Kurani kinasema juu ya visa kama hivyo:





“Na mtakapo  wapa wanawake talaka, nao wakafikia kumaliza eda yao, basi warejeeni kwa wema au waachilieni kwa wema . Wala msiwarejee kwa kuwadhuru mkafanya uadui.Na atakaye fanya hivyo amejidhulumu nafsi yake.” (Kurani 2:231, tazama pia 2:229 and 33:49)





(6)  Kuhusisha mitala kwenye Uislamu, kana kwamba ulianzishwa na hiyo au ni desturi  kulingana na mafundisho yake, ni moja wapo ya hadithi zinazoendelea katika fasihi na vyombo vya habari vya Magharibi. Mitala ilikuwepo kwenye mataifa yote na hata ilidhinishwa na Uyahudi na Ukristo hadi karne za hivi karibuni. Uislamu haukukataza ndoa ya wake wenza  kama vile ilipingwa na watu wengi na jamii za kidini; badala yake, iliidhibitiwa  na kuwekewa mipaka. Haihitajiki lakini inaruhusiwa tu kwa masharti (tazama Kurani 4: 3). Roho ya kisheria, pamoja na wakati wa kufichua dini iliyoletwa na Mungu, ili kushughulika na dharura za kibinafsi na za pamoja ambazo zinaweza kutokea mara kwa mara (kwa mfano usawa kati ya idadi ya wanaume na wanawake iliyoundwa na vita) na kutoa suluhisho la uadilifu, vitendo, na suluhu za kibinadamu kwa kuangazia shida za wajane na yatima.





C)        Kama Mama:


(1) Kurani imeinua fadhila kwa wazazi (hasa mama) kwa hali ya pili baada ya ibada ya Mungu:





“ Na Mola wako Mlezi ameamrisha kuwa msimuabudu yeyote ila Yeye tu, na wazazi wawili muwatendee wema. Mmoja wao akifikia uzee, naye yuko kwako, au wote wawili, basi usimwambie hata ah! Wala usiwakemee. Na sema nao kwa msemo wa heshima. Na uwainamishie  bawa la unyenyekevu kwa kuwaonea huruma. Na useme: Mola wangu Mlezi! Warehemu kama walivyo nilea utotoni’” (Kurani 17:23-24, tazama pia 31:14, 46:15, na 29:8)





(2)  Kwa kawaida, Mtume Muhammad alielezea tabia hii kwa wafuasi wake, akiwapa akina mama hali isiyo kifani katika uhusiano wa kibinadamu. Mtu mmoja alimjia Mtume Muhammad na kusema, “Ewe Mtume wa Mungu! Ni nani kati ya watu anayestahiki urafiki wangu mzuri?” Mtume akasema: "Mama yako." Yule mtu akasema, "Basi nani?" Mtume akasema: "Halafu mama yako." Mtu huyo aliuliza tena, "Basi nani?" Mtume akasema: "Halafu mama yako." Yule mtu akauliza tena, "Basi nani?" Mtume akasema: "Halafu baba yako."





D)        Kama Dada katika Imani (Kwa ujumla):


(1)  Kulingana na maneno ya Mtume Muhammad: "wanawake ni shaqa'iq (mapacha nusu ama dada) wa wanaume." Msemo huu ni taarifa nzito ambayo inahusiana moja kwa moja na suala la usawa wa binadamu kati ya jinsia. Ikiwa maana ya kwanza ya neno la Kiarabu shaqa’iq, "nusu mapacha," linapitishwa, inamaanisha kuwa mwanamume ana thamani ya nusu (ya jamii), wakati mwanamke anastahili nusu nyingine. Ikiwa maana ya pili, "dada," imepitishwa, inamaanisha sawa.





(2)  Mtume Muhammad alifundisha fadhila, utunzaji, na heshima kwa wanawake kwa jumla: "Ninakupongeza kuwa mzuri kwa wanawake." Ni muhimu kwamba mafundisho hayo ya Mtume yalikuwa miongoni mwa maagizo na mawaidha yake ya mwisho katika hotuba ya kuaga hijja iliyotolewa muda mfupi kabla ya kifo chake.





(3)  Staha na mwingiliano wa kijamii: Vigezo vya staha sahihi kwa wanaume na wanawake (mavazi na tabia) hutegemea vyanzo vya ufunuo (Kurani na maneno ya Mtume) na, kwa hivyo, huzingatiwa na wanaume na wanawake wanaoamini kama miongozo halali ya Mwenyezi Mungu yenye malengo na hekima. Sio vikwazo kwa  wanaume ama kwa kijamii. Inafurahisha kujua kwamba hata Biblia inahimiza wanawake kufunika kichwa: "Ikiwa mwanamke hafuniki kichwa chake, anapaswa kukatwa nywele zake; na ikiwa ni aibu kwa mwanamke kunyolewa au kunyolewa, anapaswa kufunika kichwa chake.” (1 Wakorintho 11: 6).





Nyanja ya Kisheria na Kisiasa ya Wanawake katika Uislamu


(1)  Usawa mbele ya Sheria: Jinsia zote zina haki ya usawa mbele ya Sheria na korti za Sheria. Haki haina jinsia (tazama Kurani 5:38, 24: 2, na 5:45). Wanawake wanamiliki taasisi huru za kisheria katika maswala ya kifedha na mambo mengine.





(2)  Ushiriki katika Maisha ya Kijamii na Kisiasa: Kanuni ya jumla katika maisha ya kijamii na kisiasa ni ushiriki na ushirikiano wa wanaume na wanawake katika maswala ya umma (tazama Kurani 9:71). Kuna ushahidi wa kutosha wa kihistoria wa ushiriki wa wanawake wa Kiislamu katika uchaguzi wa watawala, katika maswala ya umma, katika utengenezaji wa Sheria, katika nafasi za utawala, katika usomi na ualimu, na hata kwenye uwanja wa vita. Uhusika kama huo katika maswala ya kijamii na kisiasa ulifanywa bila washiriki kupoteza maoni ya vipaumbele vya ziada vya jinsia zote na bila kukiuka miongozo ya Kiislamu ya upole na fadhila.





Hitimisho


Hadhi ambayo wanawake wasio Waislamu wamefikia wakati huu haikupatikana kwa sababu ya huruma ya wanaume au kwa sababu ya maendeleo ya asili. Ilifanikiwa kwa njia ya mapambano marefu na kujitolea kwa upande wa mwanamke na ni wakati tu jamii ilipohitaji mchango wake na kazi, haswa wakati wa vita viwili  vya ulimwengu, na kwa sababu ya kuongezeka kwa mabadiliko ya kiteknolojia. Wakati katika Uislamu hadhi kama hiyo ya huruma na heshima iliamriwa, si kwa sababu inaonyesha mazingira ya karne ya saba, wala chini ya tishio au shinikizo la wanawake na mashirika yao, lakini kwa sababu ya ukweli wake wa ndani.





Ikiwa hii inaonyesha chochote, itaonyesha asili ya Kiungu cha kitabu kitakatifu cha Kurani na ukweli wa ujumbe wa Uislamu, ambao, tofauti na falsafa za wanadamu na itikadi, ilikuwa mbali na mazingira yake ya kibinadamu; ujumbe ambao ulianzisha kanuni kama hizi za kibinadamu ambazo hazikua zimepitwa na wakati wa wakati, na haziwezi kuzimwa wakati ujao. Baada ya yote, huu ni ujumbe wa Mungu mwenye Hekima na mwenye kujua mambo yote ambaye hekima na maarifa yake ni zaidi ya fikira na maendeleo ya mwanadamu.





 





Toa maoni



Machapisho ya hivi karibuni

FADHILA YA KUFUNGA SI ...

FADHILA YA KUFUNGA SIKU SITA ZA SHAWAL

Masuala kumi muhimu n ...

Masuala kumi muhimu na mafupi kuhusu mwezi wa Muharram

UJUMBE KWA ALIYEICHOM ...

UJUMBE KWA ALIYEICHOMA KURANI

KWANINI UISLAMU? UZU ...

KWANINI UISLAMU? UZURI NA FAIDA ZA UISLAMU