Nakala

Mmoja wa manabii wanaopewa kipaumbele zaidi katika Quran ni nabii Ibrahimu. Quran inaeleza juu yake na imani yake isiyo na shaka juu ya Mwenyezi Mungu, kwanza ikimuita kuwakataa watu wake na ibada yao ya masanamu, na baadae kuthibitisha kuwa ni mkweli kwa mitihani mbalimbali ambayo Mungu huweka mbele yake.





Katika Uislamu, Ibrahimu anaonekana kama muamini Mungu mmoja madhubuti ambaye anawaita watu wake kwenye ibada ya Mungu pekee. Kwa imani hii, anavumilia matatizo makubwa, hata kujitenga na familia yake na watu kwa njia ya kuhamia nchi mbalimbali. Yeye ni yule anayezitimiza amri mbalimbali za Mungu ingawa yeye alijaribiwa, akithibitisha kila moja kuwa kweli.





Kutokana na nguvu hii ya imani, Quran inaitaja dini moja ya kweli kuwa ni "Njia ya Ibrahimu", ingawa manabii wa kabla yake, kama vile Nuhu, waliitwa kwenye imani hiyo hiyo. Kwa sababu ya kitendo chake cha utiifu bila kuchoka kwa Mwenyezi Mungu, alimpa cheo maalum cha “Khaleel”, au mtumishi mpendwa, ambacho hakupewa Nabii mwingine yeyote hapo kabla. Kwa ubora wa Ibrahimu, Mwenyezi Mungu akawafanya Manabii kutoka kwenye kizazi chake, kutoka kwao Ismaili Isaka, Yakobo (Izraili) na Musa, wanaowaongoza watu kwenye haki.





Hadhi ya juu ya Ibrahimu inashirikiwa kwa usawa na Uyahudi, Ukristo na Uislamu. Wayahudi wanamwona kuwa ni mfano wa wema alipotimiza amri zote ingawa kabla hazijafunuliwa, na alikuwa wa kwanza kufika kwenye utambuzi wa Mungu Mmoja wa Kweli. Anaonekana kama baba wa kizazi teule, baba wa manabii kutokana na kwamba Mungu alianzisha mfululizo wake wa mafunuo. Katika Ukristo, anaonekana kama baba wa waamini wote (Warumi 4:11) na imani yake kwa Mungu na sadaka inachukuliwa kama kielelezo kwa watakatifu wa baadaye (Waebrania 11).





Kwa vile Ibrahimu anapewa umuhimu huo, inafaa mtu asome maisha yake na kuchunguza yale mambo ambayo yalimuinua hadi kufikia kiwango ambacho Mungu alimpa.





Ingawa Quran na Sunnah hazitoi maelezo ya maisha yote ya Ibrahimu, zinataja mambo fulani yenye kustahiki kuzingatiwa. Kama ilivyo kwa watu wengine wa Qurani na wa Biblia, Quran na Sunnah zinaeleza kwa undani vipengele vya maisha yao kama ufafanuzi wa baadhi ya imani potofu za dini zilizoteremshwa hapo awali, au vipengele vile ambavyo vina kauli mbiu na maadili yanayostahili kuzingatiwa na kusisitizwa.





Jina lake


Katika Quran, jina pekee alilopewa Ibrahimu ni "Ibraheem" na "Ibrahaam", zote zikishiriki mzizi asili, b-r-h-m. Ingawa katika Biblia Ibrahimu anajulikana kama Abramu mwanzoni, na kisha inasemekana Mungu alibadili jina lake na kuwa Ibrahimu, Quran imekaa kimya juu ya suala hili, bila kuthibitisha au kupinga. Wasomi wa kisasa wa Kiyahudi-Kikristo wana shaka, hata hivyo, katika hadithi ya mabadiliko ya majina yake na maana zao, wakiita "mchezo maarufu wa ulimwengu". Wanaasuria wanapendekeza kwamba herufi ya Kiebrania Hê (h) katika lahaja ya Minnean imeandikwa badala ya neno refu ‘a’ (ā), na kwamba tofauti kati ya Abrahamu na Abramu ni lahaja tu.[1] Vile vile inaweza kusemwa kwa majina ya Sarai na Sara, kwa kuwa maana zake pia zinafanana.[2]





Nchi Yake


Ibrahimu anakadiriwa kuwa alizaliwa miaka 2,166 kabla ya Yesu katika au karibu na Mesopotamia[3]  jiji la Uru[4], maili 200 kusini mashariki mwa Baghdad ya sasa[5].  Baba yake alikuwa ‘Aazar’, ‘Terah’ au ‘Terakh’ katika Biblia, mwabudu sanamu, ambaye alitokana na uzao wa Shemu, mwana wa Nuhu. Baadhi ya wasomi wa ufafanuzi wanapendekeza kwamba huenda aliitwa Azar kutokana na sanamu alilokuwa amejitolea kwake.[6]  Yaelekea alikuwa Mkadiani, watu wa Kisemiti kutoka Rasi ya Arabia walioishi Mesopotamia wakati fulani katika milenia ya tatu KK.





Inaonekana kana kwamba Azar alihama pamoja na baadhi ya jamaa zake hadi mji wa Harani katika utoto wa mapema wa Ibrahimu kabla ya kutofautiana na watu wake, ingawa baadhi ya mapokeo ya Kiyahudi-Kikristo[7]  yanasema kuwa ni baadaye katika maisha yake baada ya yeye kukataliwa katika mji wake wa asili. Katika Biblia, Harani, mmoja wa ndugu za Ibrahimu inasemekana alikufa huko Uru, “katika nchi aliyozaliwa” (Mwanzo 11:28), lakini alikuwa mkubwa zaidi kuliko Ibrahimu, kama vile ndugu yake mwingine Nahori alimchukua binti wa Harani kama mke (Mwanzo 11:29). Biblia pia haitaji kuhama kwa Ibrahimu kwenda Harani, bali amri ya kwanza ya kuhama ni ile ya kutoka Harani, kana kwamba walikuwa wamekaa huko hapo awali (Mwanzo 12: 1-5). Ikiwa tutachukua amri ya kwanza kumaanisha kuhama kutoka Uru hadi Kanaani, inaonekana hakuna sababu yoyote kwa Ibrahimu kukaa na familia yake huko Harani, na kumwacha baba yake huko na kwenda Kanaani baadaye, bila kutaja kutowezekana kwake kwa kijiografia [Angalia ramani].





Quran inataja kuhama kwa Ibrahimu, lakini inafanya hivyo baada ya Ibrahimu kujitenga na baba yake na watu wa kabila lake kutokana na ukafiri wao. Ikiwa angekuwa Uru wakati huo, inaonekana kwamba baba yake asingeenda pamoja naye hadi Harani baada ya kutoamini na kumtesa pamoja na watu wa mji wake. Kuhusu ni kwa nini walichagua kuhama, ushahidi wa kiakiolojia unapendekeza kwamba Uru ulikuwa mji mkuu ambao ulishuhudia kuinuka na kuanguka katika maisha ya Ibrahimu[8], hivyo wanaweza kuwa walilazimika kuondoka kutokana na ugumu wa mazingira. Huenda waliichagua Harani kwa sababu ya kua na dini sawa na Uru[9].





Dini ya Mesopotamia


Uvumbuzi wa kiakiolojia wa wakati wa Ibrahimu unatoa picha wazi ya maisha ya kidini ya Mesopotamia. Wakazi wake walikuwa washirikina walioamini katika miungu, ambapo kila mungu alikuwa na nyanja ya ushawishi. Hekalu kubwa liliwekwa kwa Akkadian[10] mungu wa mwezi, Sin, ilikuwa kituo kikuu cha Uru. Harani pia ilikuwa na mwezi kama mungu mkuu. Hekalu hili liliaminika kuwa nyumba ya kimwili ya Mungu. Mungu mkuu wa hekalu alikuwa sanamu ya mbao yenye sanamu zingine, au ‘miungu’, ili kumtumikia.





Ziggurati Mkuu wa Uru, hekalu la mungu wa mwezi Nanna, anayejulikana pia kama Sin. Ilipigwa mwaka 2004, picha hiyo ni kwa hisani ya Lasse Jensen.


Maarifa ya Mungu


Ingawa wanazuoni wa Kiyahudi-Kikristo wametofautiana kuhusu lini Ibrahimu alikuja kumjua Mungu, akiwa na umri wa miaka mitatu, kumi, au arobaini na nane[11], Quran iko kimya katika kutaja umri kamili ambao Ibrahimu alipokea ufunuo wake wa kwanza. Inaonekana, ilikuwa, hata hivyo, alipokuwa mdogo katika umri, kwa vile Quran inamuita kijana wakati watu wake wanajaribu kumuua kwa kukataa masanamu yao, na Ibrahimu mwenyewe alisema kuwa hakuwa na ufahamu kwa baba yake wakati alipomuita kumwabudu Mungu peke yake kabla wito wake haujaenea kwa watu wake (19:43). Quran iko wazi, hata hivyo, kwa kusema kwamba alikuwa ni mmoja wa Mitume waliofunuliwa Kitabu:





"Hakika haya yamo katika Vitabu vya mwanzo,  Vitabu vya Ibrahimu na Musa." (Quran 87:18-19)





Kisha wakati ukafika ambapo mahubiri ilibidi yaambatane na matendo halisi. Ibrahimu alipanga pigo la ujasiri na la maamuzi katika ibada ya sanamu. Maelezo ya Quran ni tofauti kidogo na yale yanayotajwa katika mila za Kiyahudi-Kikristo, kama yanavyosema kwa Ibrahimu kuharibu sanamu binafsi za baba yake.[1]  Quran inasema kwamba aliharibu masanamu ya watu wake, yaliyowekwa kwenye madhabahu ya kidini. Ibrahimu alikuwa amedokeza mpango unaohusisha masanamu:





"Na Wallahi! Nitayafanyia vitimbi masanamu yenu haya baada ya mkisha geuka kwenda zenu." (Quran 21:57)





Ulikuwa ni wakati wa sikukuu ya kidini, labda iliwekwa kwa ajili ya Sin, ambao walitoka nje ya mji. Ibrahimu alialikwa kuhudhuria sikukuu hiyo, lakini akaomba radhi,





""Na akatazama kwenye nyota. Kisha akasema: 'Hakika! Najisikia mgonjwa!'’"





Kwa hiyo, wakati wenzake waliondoka bila yeye, ikawa fursa yake. Hekalu lilipoachwa, Ibrahimu alienda huko na kukaribia sanamu za mbao zilizopakwa dhahabu, ambazo zilikuwa na vyakula vingi viliyoachwa mbele yao na makuhani. Ibrahimu akawakejeli kwa ukafiri.





"Kisha akaigeukia miungu yao na kusema: 'Je, hautokula? Una shida gani hata husemi?’”





Kwani, ni nini kingeweza kumdanganya mwanadamu kuabudu miungu ya vinyago vyake mwenyewe?





"Kisha akavishambulia, akiwapiga kwa mkono wake wa kulia."





Quran inatuambia:





"Basi akayavunja vipande vipande, ila kubwa lao."





Makuhani wa hekalu waliporudi, walishtuka kuona kufuru, uharibifu wa hekalu. Walikuwa wanashangaa ni nani angeweza kufanya hivi kwa sanamu zao wakati mtu alitaja jina la Ibrahimu, akieleza kwamba alikuwa akiwasema vibaya. Walipomwita mbele yao, ilikuwa ni kwa Ibrahimu kuwaonyesha upumbavu wao:





"Akasema: ‘Muabuduni mnachokichonga wakati Mwenyezi Mungu amekuumbeni nyie na icho mnacho kitengeneza?'"





Hasira yao ilikuwa inaongezeka; bila kuhubiriwa, walifika moja kwa moja kwenye jambo hilo:





"Wakasema: Je! Wewe umeifanyia haya miungu yetu, ewe Ibrahim?"





Lakini Ibrahimu alikuwa ameacha sanamu kubwa bila kuguswa kwa sababu:





"Akasema: Bali amefanya hayo huyu mkubwa wao. Basi waulizeni ikiwa wanaweza kutamka!’"





Ibrahimu alipowapinga hivyo, waliingiwa na mkanganyiko. Wakalaumiana wao kwa wao kwa kutoyalinda masanamu na wakakataa kukutana na macho yake, wakasema:





"Kweli unajua vizuri hawa hawasemi!"





Kwa hiyo Ibrahimu akasisitiza kesi yake.





"Akasema: Basi nyinyi mnawaabudu asiye kuwa Mwenyezi Mungu wasio kufaini kitu wala kukudhuruni? Aibu yenu nyinyi na hivyo mnavyo viabudu badala ya Mwenyezi Mungu! Basi nyinyi hamtii akilini?’"





Washtaki wakawa washtakiwa. Walishutumiwa kwa kutofautiana kimantiki, na hivyo hawakuwa na jibu kwa Ibrahimu. Kwa sababu mawazo ya Ibrahimu hayakuwa na majibu, jibu lao lilikuwa hasira na ghadhabu, na walimhukumu Ibrahamu kuchomwa moto akiwa hai,





"Mjengee jengo na umtupe kwenye moto mwekundu."





Watu wa mjini walisaidia kukusanya kuni kwa ajili ya moto huo, hadi ukawa moto mkubwa zaidi kuwahi kutokea. Kijana Ibrahimu alinyenyekea kwenye majaaliwa aliyochaguliwa na Mola Mlezi wa walimwengu wote. Hakupoteza imani, bali jaribio hilo lilimfanya awe na nguvu zaidi. Ibrahimu hakukurupuka mbele ya kifo cha moto hata katika umri huu mdogo; badala yake maneno yake ya mwisho kabla ya kuingia humo yalikuwa,





"Mwenyezi Mungu ananitosheleza, na Yeye ndiye bora wa kusimamia mambo." (Saheeh Al-Bukhari)





Hapa tena kuna mfano wa Ibrahimu aliyethibitika kuwa mwaminifu kwa majaribu aliyoyakabili. Imani yake katika Mungu wa Kweli ilijaribiwa hapa, na alithibitisha kwamba alikuwa tayari hata kusitisha uwepo wake kwa wito wa Mungu. Imani yake ilithibitishwa na kitendo chake.





Mungu hakutaka kwamba hii iwe hatima ya Ibrahimu, kwa kuwa alikuwa na utume mkubwa mbele yake. Alipaswa kuwa baba wa baadhi ya manabii wakuu wanaojulikana kwa wanadamu. Mungu alimuokoa Ibrahimu kama ishara kwake na kwa watu wake pia.





“Sisi tukasema: 'Ewe moto! Kuwa baridi na salama kwa Ibrahim!’ Na wakataka kumtegea mtego, lakini tukawafanya wao kuwa wenye hasara zaidi.





Hivyo Ibrahimu aliuepuka moto, bila kudhurika. Walijaribu kulipiza kisasi kwa ajili ya miungu yao, lakini wao na sanamu zao mwishowe walidhalilishwa.





Ibrahimu ndani ya Kanaani na Misri


Ibrahimu alikaa Kanaani kwa miaka kadhaa akienda jiji hadi jiji akihubiri na kuwaalika watu kwa Mungu hadi njaa ilipomlazimisha yeye na Sara kuhamia Misri. Huko Misri kulikuwa na Firauni mdhalimu ambaye alitamani sana kuwamiliki wanawake walioolewa.[1]  Maelezo haya ya Kiislamu ni tofauti kabisa na mila za Kiyahudi-Kikristo, ambayo yanasema kwamba Ibrahimu alidai kwamba Sara[2]  alikuwa dada yake ili kujiokoa kutoka kwa Firauni.[3].  Firauni akamchukua Sara katika nyumba yake na akamtukuza Ibrahimu kwa ajili yake, lakini nyumba yake ilipokumbwa na magonjwa makali, alikuja kujua kwamba alikuwa ni mke wa Ibrahimu na akamwadhibu kwa kutomwambia hivyo, hivyo kumfukuza kutoka Misri.[4]





Ibrahimu alijua kwamba Sara angevuta hisia zake, kwa hiyo akamwambia kwamba ikiwa Firauni angemuuliza, aseme kwamba yeye ni dada wa Ibrahimu. Walipoingia katika ufalme wake, kama ilivyo tarajiwa, Firauni aliuliza kuhusu uhusiano wake na Sara, na Ibrahimu akajibu kwamba alikuwa dada yake. Ingawa jibu hilo lilipunguza mapenzi yake, bado alimchukua mateka. Lakini ulinzi wa Mwenyezi Mungu ulimuokoa na njama yake mbaya. Firauni alipomwita Sara ili atende kulingana na tamaa zake za kiakili, Sara alimgeukia Mungu katika sala. Mara tu Firauni alipomfikia Sara, sehemu yake ya juu ya mwili ulikakamaa. Alimlilia Sara kwa huzuni, akiahidi kumwachilia ikiwa angemuombea apone! Aliomba kuachiliwa kwake. Lakini tu baada ya jaribio la tatu lililoshindwa ndipo hatimaye aliacha. Kwa kutambua hali yao ya pekee, alimruhusu aende na kumrudisha kwa aliyedhaniwa kuwa kaka yake.





Sara alirudi wakati Ibrahimu alipokuwa akiomba, akisindikizwa na zawadi kutoka kwa Farao, kwa vile alikuwa ametambua hali yao maalumu, pamoja na binti yake mwenyewe Hagari pia, kulingana na mapokeo ya Kiyahudi-Kikristo, kama mjakazi[5].  Alikuwa ametoa ujumbe wenye nguvu kwa Firauni na Wamisri wapagani.





Baada ya kurudi Palestina, Sara na Ibrahimu waliendelea kutokuwa na mtoto, licha ya ahadi za Mungu kwamba angepewa mtoto. Zawadi ya mjakazi ka mwanamke tasa kwa mumewe ili kuzaa inaonekana kuwa jambo la kawaida nyakati hizo[6], Sara alipendekeza kwa Ibrahimu kwamba amchukue Hajiri kama hawara wake. Baadhi ya wasomi wa Kikristo wanasema kuhusu tukio hili kwamba alimchukua kama mke wake[7].  Vyovyote itakavyokuwa, katika mila ya Wayahudi na Wababiloni, mtoto yoyote aliyezaliwa na hawara angekuwa ni wa bibi wa zamani wa hawara huyo na kutendewa sawa sawa kabisa na mtoto aliyezaliwa naye[8], ikiwemo masuala ya urithi. Akiwa Palestina, Hajari alimzalia mtoto wa kiume, Ishmaeli





Ibrahimu ndani ya Makka


Ishmaeli alipokuwa bado ananyonya, Mungu alichagua tena kuijaribu imani ya mpendwa wake Ibrahimu na kumwamuru awapeleke Hagari na Ishmaeli hadi kwenye bonde lisilo na maji la Bakka maili 700 kusini-mashariki mwa Hebroni. Katika nyakati za baadaye ingeitwa Makka. Hakika ulikuwa mtihani mkubwa sana, kwani yeye na familia yake walikuwa wametamani sana wakati huo wa uzao, na macho yao yalijawa na furaha ya kua na mrithi, amri iliwekwa ya kumpeleka katika nchi ya mbali, inayojulikana kwa utasa na shida.





Ingawa Quran inathibitisha kwamba hii ilikuwa mtihani mwingine kwa Ibrahimu wakati Ishmaeli angali mtoto mchanga, Biblia na mapokeo ya Kiyahudi-Kikristo yanadai kwamba ilikuwa ni matokeo ya hasira ya Sara, ambaye alimwomba Ibrahimu kumfukuza Hajari na mwanawe alipoona Ishmaeli "akimdhihaki"[9]  Isaka[10]  baada ya kuachishwa kunyonya. Kwa kuwa umri wa kawaida wa kuachishwa kunyonya, katika utamaduni wa Kiyahudi angalau , ulikuwa miaka 3[11], hii inadokeza kwamba Ishmaeli alikuwa na takriban miaka 17[12] tukio hili lilipotokea. Inaonekana kimantiki kuwa haiwezekani, kwamba Hajiri angeweza kumbeba mwanaume kijana mabegani mwake na kumpeleka kwa mamia ya maili hadi alipofika Parani, kisha tu kumlaza, kama Biblia inavyosema, chini ya kichaka[13]. Katika aya hizi Ishmaeli anatajwa kwa neno tofauti na lile lililotumika kuelezea kufukuzwa kwake. Neno hili linaonyesha kwamba alikuwa mvulana mdogo sana, labda mtoto, badala ya kijana.





Kwa hiyo Ibrahimu, baada ya kukaa pamoja na Hajari na Ishmaeli, akawaacha huko wakiwa na kiriba cha maji na mfuko wa ngozi uliojaa tende. Ibrahimu alipoanza kuondoka akiwaacha nyuma, Hagari akawa na wasiwasi juu ya kile kilichokuwa kikitendeka. Ibrahimu hakutazama nyuma. Hajari akamkimbilia, ‘Ewe Ibrahimu, unakwenda wapi, ukituacha katika bonde hili ambapo hakuna mtu ambaye tunaweza kufurahia ushirika wake, wala hakuna kitu hapa?’’





Ibrahimu aliharakisha mwendo wake. Hatimaye, Hagari akauliza, ‘Je, Mungu amekuomba ufanye hivyo?’





Ghafla, Ibrahimu akasimama, akageuka nyuma na kusema, ‘Ndiyo!’





Akihisi faraja kwa kadiri fulani katika jibu hili, Hagari aliuliza, ‘Ee Ibrahimu, unatuacha kwa nani?’





‘Nina kuacha chini ya uangalizi wa Mungu,’ Ibrahimu akajibu.





Hajiri alijisalimisha kwa Mola wake Mlezi, ‘Nimetosheka kuwa pamoja na Mwenyezi Mungu!’[14]





Alipokuwa akifuatilia njia yake ya kurudi kwa Ishmaeli mdogo, Ibrahimu aliendelea mpaka akafika kwenye njia nyembamba mlimani ambapo hawangeweza kumwona. Alisimama hapo na kumwomba Mungu kwa maombi:





"Mola wetu Mlezi! Hakika mimi nimewaweka baadhi ya dhuriya zangu katika bonde lisilo kuwa na mimea, kwenye Nyumba yako Takatifu, ewe Mola wetu Mlezi, ili washike Swala. Basi zijaalie nyoyo za watu zielekee kwao, na waruzuku matunda, ili wapata kushukuru" (Quran 14:37)





Punde, maji na tende zilikwisha na kukata tamaa kwa Hajari kuliongezeka. Kwa kuwa hakuweza kuzima kiu yake au kumnyonyesha mtoto wake mdogo, Hagari alianza kutafuta maji. Akimuacha Ishmaeli chini ya mti, alianza kupanda mteremko wa mawe wa mlima uliokuwa karibu. ‘Labda kuna msafara unapita,’ alijiwazia. Alikimbia kati ya vilima viwili vya Safa na Marwa mara saba akitafuta dalili za maji au msaada, ambapo baadaye zilifananishwa na Waislamu wote katika Hijja. Akiwa amechoka na kufadhaika, alisikia sauti, lakini hakuweza kupata chanzo chake. Kisha, akitazama chini kwenye bonde, alimwona malaika, ambaye anajulikana kama Gabrieli katika vyanzo vya Kiislamu[15], amesimama karibu na Ishmaeli. Malaika akachimba ardhini kwa kisigino chake karibu na mtoto mchanga, na maji yakatoka. Ilikuwa ni muujiza! Hajari alijaribu kutengeneza beseni kulizunguka ili yasitirike nje, na akajaza chombo chake.[16]  'Msiogope kuachwa,” Malaika akasema, ‘maana hii ndiyo Nyumba ya Mungu itakayojengwa na kijana huyu na baba yake, na Mungu kamwe hawapuuzi watu wake.’[17]  Kisima hiki kiitwacho Zamzam kinatiririka hadi leo katika mji wa Makka katika Rasi ya Uarabuni.





Haikupita muda mrefu baadaye, kabila la Jurham, likihama kutoka kusini mwa Arabia, lilisimama karibu na bonde la Makka baada ya kuona muonekano usio wa kawaida wa ndege akiruka upande wake, ambayo inaweza kumaanisha uwepo wa maji tu. Hatimaye waliishi Makka na Ismail akakua miongoni mwao.





Simulizi kama hilo la kisima hiki limetolewa katika Biblia katika Mwanzo 21. Katika simulizi hili, sababu ya kumuacha mtoto mchanga ilikuwa ni kuepuka kumwona akifa badala ya kutafuta msaada. Kisha, baada ya mtoto huyo kuanza kulia kwa kiu, alimwomba Mungu amwondoe asimwone akifa. Kuonekana kwa kisima hicho kulisemekana kuwa ni kuitikia kilio cha Ishmaeli, badala ya dua yake, na hakuna jitihada zozote kutoka kwa Hajari kutafuta msaada zinazoripotiwa hapo. Pia, Biblia inaeleza kwamba kisima hicho kilikuwa katika nyika ya Parani, ambako walikaa baadaye. Wasomi wa Kiyahudi-Kikristo mara nyingi hutaja kwamba Parani iko mahali fulani kaskazini mwa Rasi ya Sinai, kutokana na kutajwa kwa Mlima Sinai katika Kumbukumbu ya Torati 33:2. Wanaakiolojia wa kisasa wa kibiblia, hata hivyo, wanasema kwamba Mlima Sinai kwa hakika uko katika Saudi Arabia ya kisasa, jambo ambalo linalazimu Parani iwe huko pia.[18]


Ibrahimu Amtoa Sadaka Mwanawe


Ilikuwa imekaribia miaka kumi tangu Ibrahimu kumwacha mke wake na mtoto huko Makka chini ya uangalizi wa Mungu. Baada ya safari ya miezi miwili, alishangaa kukuta Makka tofauti na jinsi alivyoiacha. Furaha ya kuungana tena ilikatizwa haraka na maono ambayo ingekuwa jaribu kuu la imani yake. Mungu alimwamuru Ibrahimu kupitia ndoto amtoe sadaka mwanawe, mwana ambaye alikuwa naye baada ya miaka mingi ya maombi na ndo alikuwa amekutana naye baada ya miaka kumi ya kutengana.





Tunajua kutoka katika Quran kwamba mtoto atakayetolewa sadaka alikuwa Ismaili, Mungu, wakati wa kutoa habari njema ya kuzaliwa kwa Isaka kwa Ibrahimu na Sara, pia alitoa habari njema ya mjukuu, Yakobo (Israeli):





"…Basi tukambashiria (kuzaliwa) Is-haq, na baada ya Is-haq Yaaqub." (Quran 11:71)





Vile vile, katika mstari wa Biblia Mwanzo 17:19, Ibrahimu aliahidiwa:





"Sara mkeo atakuzalia mwana ambaye jina lake litakuwa Isaka. Nitalithibitisha agano langu naye kuwa agano la milele na uzao wake baada yake."





Kwa sababu Mungu aliahidi kumpa Sara mtoto kutoka kwa Ibrahimu na wajukuu kutoka kwa mtoto huyo, kwa kimantiki wala kimatendo haiwezekani kwa Mungu kumwamuru Ibrahimu amtoe sadaka Isaka, kwa kuwa Mungu havunji ahadi yake, wala Yeye si "mwandishi wa kuchanganya."





Ingawa jina la Isaka linatajwa wazi wazi kuwa ndiye ambaye angetolewa sadaka katika Mwanzo 22:2, tunajifunza kutokana na muktadha mwingine wa Biblia kwamba ni tafsiri ya wazi, na aliyepaswa kuchinjwa alikuwa Ishmaeli.





"Mwanao wa Pekee"


Katika mistari ya Mwanzo 22, Mungu anamwamuru Ibrahimu amtoe sadaka mwanawe wa pekee. Wanazuoni wote wa Uislamu, Uyahudi na Ukristo wanakubali, Ishmaeli alizaliwa kabla ya Isaka. Kutokana na hili, haingefaa kumwita Isaka mwana wa pekee wa Ibrahimu.





Ni kweli kwamba wasomi wa Kiyahudi-Mkristo mara nyingi hubishana kwamba kwa kuwa Ishmaeli alizaliwa na hawara, yeye si mwana halali. Hata hivyo, tayari tumeshataja hapo awali kwamba kwa mujibu wa Dini ya Kiyahudi, kuwapa waume zao mahawara kutoka kwa wake tasa ili wazae watoto lilikuwa jambo la kawaida, lililo halali na linalokubalika, na mtoto aliyezaliwa na hawara huyo angekua wa mke wa baba[1], kufurahia haki zote kama yeye, wa mke, mtoto wake mwenyewe, ikiwa ni pamoja na urithi. Zaidi ya hayo, wangepokea sehemu maradufu ya watoto wengine, hata kama "wangechukiwa"[2].





Zaidi ya hayo, imedokezwa katika Biblia kwamba Sara mwenyewe angemwona mtoto aliyezaliwa na Hajiri kuwa mrithi halali. Akijua kwamba Ibrahimu alikuwa ameahidiwa kwamba uzao wake ungeijaza nchi kati ya Mto Nile na Frati (Mwanzo 15:18) kutoka katika mwili wake mwenyewe (Mwanzo 15:4), alimtoa Hajiri kwa Ibrahimu ili awe njia ya kutimiza unabii huu. Alisema,





“Tazama sasa, Bwana amenizuia kuzaa; nakusihi, uingie kwa mjakazi wangu; labda ninaweza kupate watoto kupitia kwake” (Mwanzo 16:2). (Mwanzo 16:2)





Hii pia ni sawa na Lea na Raheli, wake za Yakobo mwana wa Isaka, kumpa Yakobo vijakazi wao ili wazae watoto (Mwanzo 30:3, 6. 7, 9-13). Watoto wao walikuwa Dani, Neftali, Gadi na Asheri, ambao walitoka kwa wana kumi na wawili wa Yakobo, baba wa makabila kumi na mawili ya Waisraeli, na kwa hivyo ni warithi halali[3].





Kutokana na hili, tunaelewa kwamba Sara aliamini kwamba mtoto aliyezaliwa na Hajari angekuwa utimilifu wa unabii aliopewa Ibrahimu, na kuwa kana kwamba alizaliwa kwa nafsi yake mwenyewe. Hivyo, kulingana na ukweli huu pekee, Ishmaeli si haramu, bali ni mrithi halali.





Mungu Mwenyewe anamchukulia Ishmaeli kama mrithi halali, kwa maana, katika sehemu nyingi, Biblia inataja kwamba Ishmaeli ni "uzao" wa Ibrahimu. Kwa mfano, katika Mwanzo 21:13:





“Tena mwana wa mjakazi nitamfanya taifa, kwa maana yeye ni uzao wako.





Kuna sababu nyingine nyingi zinazo thibitisha kwamba ni Ishmaeli na sio Isaka ambaye angetolewa sadaka, na mapenzi ya Mungu, makala tofauti zitawekwa kwa ajili ya suala hili.





Kwa kuendelea na simulizi hili, Ibrahimu alishauriana na mwanawe ili kuona kama alielewa kile alichoamriwa na Mungu,





"Basi tukambashiria mwana aliye mpole. Basi alipo fika makamo ya kwenda na kurudi pamoja naye, alimwambia: Ewe mwanangu! Hakika mimi nimeona usingizini kuwa ninakuchinja. Basi angalia wewe, waonaje? Akasema: Ewe baba yangu! Tenda unavyo amrishwa, utanikuta mimi, Inshallah, katika wanao subiri." (Quran 37:101-102)





Kwa hakika mtu akiambiwa na baba yake kwamba atauawa kwa sababu ya ndoto, haitachukuliwa kwa adabu njema. Mtu anaweza kutilia shaka ndoto hiyo pamoja na utimamu wa mtu huyo, lakini Ishmaeli alijua hali ya baba yake. Mtoto mchamungu wa baba mcha Mungu alijitolea kujisalimisha kwa Mungu. Ibrahimu akampeleka mwanawe mahali ambapo angetolewa sadaka na akamlaza kifudifudi. Kwa sababu hii, Mungu amewaeleza kwa maneno mazuri sana, akichora taswira ya kiini cha utii; ambayo huleta machozi kwa macho:





"Basi wote wawili walipo jisalimisha, na akamlaza juu ya kipaji." (Quran 37:103)





Kisu cha Ibrahimu kilipokuwa karibu kushuka, sauti ilimzuia





"Tulimwita: Ewe Ibrahim: Umekwisha itimiliza ndoto. Hakika hivi ndivyo tunavyo walipa wanao tenda mema.   Hakika haya ni majaribio yaliyo dhaahiri." (Quran 37:104-106)





Hakika ulikuwa mtihani mkubwa kuliko yote, kumtoa sadaka mtoto wake wa pekee, aliyemzaa baada ya kufikia uzee na miaka ya kutamani uzao. Hapa, Ibrahimu alionyesha nia yake ya kutoa sadaka mali yake yote kwa ajili ya Mungu, na kwa sababu hii, aliteuliwa kuwa kiongozi wa wanadamu wote, ambaye Mungu alimbariki na kizazi cha Manabii.





"Na Mola wake Mlezi alipo mjaribu Ibrahim kwa kumpa amri fulani, naye akazitimiza, akamwambia: Hakika Mimi nitakufanya uwe mwongozi wa watu. Akasema: Je, na katika vizazi vyangu pia?" (Quran 2:124)





Ishmaeli alikombolewa kwa kondoo dume,





‘…Basi tukamtolea fidia kwa dhabihu mtukufu.’ (Quran 37:107)





Ni mfano huu wa kunyenyekea na kumtegemea Mwenyezi Mungu ambao mamia ya mamilioni ya Waislamu huigiza kila mwaka katika siku za Hija, siku inayoitwa Yawm-un-Nahr – Siku ya Sadaka, au Eid-ul-Adhaa – au Sherehe ya Sadaka.





Ibrahimu alirudi Palestina, na baada ya kufanya hivyo, alitembelewa na malaika ambao walimpa yeye na Sara habari njema ya mwana, Isaka.





"Wakasema: Usiogope. Sisi tunakubashiria kijana mwenye ujuzi." (Quran 15:53)





Ni wakati huu ambapo pia anaambiwa kuhusu kuangamizwa kwa watu wa Lutu.


Ibrahimu and Ishmaeli Wajenga Kaaba


Baada ya utengano wa miaka kadhaa, baba na mwana walikutana tena. Ilikuwa katika safari hii ambapo hao wawili walijenga Kaaba kwa amri ya Mungu kama pahala patakatifu pa kudumu; pahala palipojengwa kwa ajili ya ibada ya Mungu. Ilikuwa ni hapa, katika jangwa hili ambako Ibrahimu alikuwa amewaacha Hagari na Ishmaeli hapo awali, ndipo alipomwomba Mungu apafanye mahali ambapo wangeweza kushikilia sala, na kuepukana na ibada ya sanamu.





"Na Ibrahim alipo sema: Ewe Mola wangu Mlezi! Ujaalie mji huu uwe wa amani, na uniepushe mimi na wanangu na kuabudu masanamu. Ewe Mola wangu Mlezi! Hakika hayo yamewapoteza watu wengi. Basi aliye nifuata mimi huyo ni wangu, na aliye niasi, hakika Wewe ni Mwenye kusamehe Mwenye kurehemu. Mola wetu Mlezi! Hakika mimi nimewaweka baadhi ya dhuriya zangu katika bonde lisilo kuwa na mimea, kwenye Nyumba yako Takatifu, ewe Mola wetu Mlezi, ili washike Sala. Basi zijaalie nyoyo za watu zielekee kwao, na waruzuku matunda, ili wapata kushukuru. Ewe Mola wetu Mlezi! Hakika Wewe unajua tunayo yaficha na tunayo yatangaza. Na hapana kitu kinacho fichikana kwa Mwenyezi Mungu katika ardhi wala katika mbingu. Alhamdulillahi! Himdi zote ni za Mwenyezi Mungu aliye nipa juu ya uzee wangu Ismail na Is-haq. Hakika Mola wangu Mlezi ni Mwenye kusikia maombi. Mola wangu Mlezi! Nijaalie niwe mwenye kushika Sala, na katika dhuriya zangu pia. Ewe Mola wetu Mlezi, na ipokee dua yangu. Mola wetu! Unighufirie mimi na wazazi wangu wote wawili, na Waumini, siku ya kusimama hisabu." (Kurani 14:35-41)





Miaka mingi baadaye, Ibrahimu anaungana tena na mwanawe Ishmaeli, ili waanzishe Nyumba ya Mungu iliyoheshimiwa, iwe kituo cha ibada, ambapo watu wangeelekeza nyuso zao wakisali, na kuifanya kuwa mahali pa Hija. Kuna aya nyingi nzuri katika Qurani zinazoelezea utakatifu wa Kaaba na kusudi la ujenzi wake.





"Na pale tulipomweka Ibrahim pahala penye ile Nyumba tukamwambia: Usinishirikishe na chochote; na isafishe Nyumba yangu kwa ajili ya wanao izunguka kwa kut'ufu, na wanao kaa hapo kwa ibada, na wanao rukuu, na wanao sujudu. Na watangazie watu Hija; watakujia kwa miguu na juu ya kila ngamia aliye konda, wakija kutoka katika kila njia ya mbali." (Kurani 22:26-27)





"Na kumbukeni tulipo ifanya ile Nyumba (ya Alkaaba) iwe pahala pa kukusanyikia watu na pahala pa amani. Na alipo kuwa akisimama Ibrahim pafanyeni pawe pa kusalia. Na tuliagana na Ibrahim na Ismail: Itakaseni Nyumba yangu kwa ajili ya wanao izunguka kwa kut'ufu na wanao jitenga huko kwa ibada, na wanao inama na kusujudu." (Kurani 2:125)





Kaaba ni mahali ya kwanza ya ibada iliyoteuliwa kwa ajili ya wanadamu wote kwa lengo la mwongozo na baraka:





"Hakika Nyumba ya kwanza walio wekewa watu kwa ibada ni ile iliyoko Bakka, iliyo barikiwa na yenye uwongofu kwa walimwengu wote. Ndani yake zipo Ishara zilizo wazi - masimamio ya Ibrahim, na mwenye kuingia humo anakuwa katika amani. Na kwa ajili ya Mwenyezi Mungu imewajibikia watu wahiji kwenye Nyumba hiyo, kwa yule awezae njia ya kwendea. " (Kurani 3:96-97)





Mtume Muhammad, rehema na baraka za Mwenyezi Mungu ziwe juu yake, alisema:





"Hakika Mwenyezi Mungu amepafanya patakatifu pahala hapa siku alipo ziumba mbingu na ardhi, na patakuwa hivyo mpaka Siku ya Kiyama." (Saheeh Al-Bukhari, Saheeh Muslim)





Dua za Ibrahimu


Kwa hakika, ujenzi wa pahala patakatifu patakapoheshimiwa na vizazi vyote vijavyo ulikuwa ni mojawapo ya njia bora za ibada ambazo watu wa Mungu wangeweza kufanya. Walimwomba Mwenyezi Mungu wakati wa tendo lao:





"Ewe Mola Mlezi wetu! Tutakabalie! Hakika Wewe ndiye Msikizi Mjuzi. Ewe Mola Mlezi wetu! Tujaalie tuwe ni wenye kusilimu kwako, na pia miongoni mwa vizazi vyetu wawe umma ulio silimu kwako. Na utuonyeshe njia za ibada yetu na utusamehe. Bila shaka Wewe ndiye Mwenye kusamehe Mwenye kurehemu!" (Kurani 2:127-128)





" Na alipo sema Ibrahim: Ee Mola wangu Mlezi! Ufanye huu uwe mji wa amani, na uwaruzuku watu wake matunda, wale wanao muamini Mwenyezi Mungu na Siku ya Mwisho...." (Kurani 2:126)





Ibrahimu pia aliomba kwamba nabii afufuliwe kutoka katika uzao wa Ishmaeli, ambao wangekuwa wenyeji wa nchi hii, kama vile wazao wa Isaka wangekuwa wenyeji wa nchi za Kanaani.





"Ewe Mola Mlezi wetu! Waletee Mtume anaye tokana na wao, awasomee Aya zako, na awafundishe Kitabu na hikima na awatakase. Hakika Wewe ndiye Mwenye nguvu, Mwenye hikima." (Kurani 2:127-129)





Kaabah iliyojengwa na Ibrahimu na Ishmaeli na Kituo cha Ibrahimu, ambacho kinahifadhi nyayo za Mtume Ibrahimu.


Maombi ya Ibrahimu ya kuletwa kwa Mtume yalijibiwa baada ya maelfu kadhaa ya miaka wakati Mungu alipomtoa Mtume Muhammad kutoka kwa Waarabu, na kama Makka ilivyochaguliwa kuwa patakatifu na Nyumba ya Ibada kwa wanadamu wote, hivyo pia Mtume wa Makka alitumwa kwa wanadamu wote.





Ilikuwa ni kilele hiki cha maisha ya Ibrahimu kilichokuwa kukamilika kwa lengo lake: kujenga pahala pa ibada kwa wanadamu wote, si kwa ajili ya kabila lolote au rangi, bali kwa ajili ya ibada ya Mungu Mmoja wa Kweli. Ni kupitia kuanzishwa kwa nyumba hii ndipo palikuwa dhamana ya kwamba Mungu, Mungu ambaye alimwomba na ambaye alimtolea dhabihu zisizo na mwisho, Ataabudiwa milele, bila ya kumshirikisha na miungu mingine. Hakika hii ilikuwa katika fadhila kubwa alizopewa mwanaadamu yeyote.





Ibrahimu na Hija


Kila mwaka, Waislamu kutoka duniani kote hukusanyika kutoka kwa matabaka yote ya maisha, na hilo ni jibu la maombi ya Ibrahimu na wito wa Hija. Ibada hii inaitwa Hajj, na inaadhimisha matukio mengi ya mtumishi mpendwa wa Mungu Ibrahimu na familia yake. Baada ya kuzunguka Kaaba, Mwislamu anasali nyuma ya Kituo cha Ibrahimu, jiwe ambalo Ibrahimu alisimamia kujenga Kaaba. Baada ya sala, Waislamu hunywa kutoka kwa kisima kiitwacho Zamzam, kilichotokea kama jibu la ombi la Ibrahimu na Hagar, ili kuwapa riziki Ishmaeli na Hajari, na ndiyo sababu ya watu kukaa katika nchi hiyo. Ibada ya kutembea kati ya Safaa na Marwah inaadhimisha kutafuta maji kwa Hagar wakati yeye na mtoto wake walikuwa peke yao huko Makka. Kuchinjwa kwa mnyama huko Mina wakati wa Hija, na Waislamu duniani kote katika nchi zao wenyewe wanavyofanya, ni katika kufuata mfano wa nia ya Ibrahimu ya kumtoa mwanawe kama dhabihu kwa ajili ya Mungu. Mwishowe, kupiga mawe kwa nguzo za mawe huko Mina kunaonyesha jinsi Ibrahimu alivyokataa ushawishi wa kishetani wa kumzuia kumtoa Ishmaeli kama dhabihu.





“Mtumishi mpendwa wa Mungu” ambaye Mungu alisema juu yake, "Hakika Mimi nitakufanya uwe mwongozi wa watu,,"[1]  akarudi Palestina na kufa huko.



Machapisho ya hivi karibuni

UJUMBE KUTOKA KWA MUH ...

UJUMBE KUTOKA KWA MUHUBIRI MUISLAMU KWA MKRISTO

FADHILA YA KUFUNGA SI ...

FADHILA YA KUFUNGA SIKU SITA ZA SHAWAL

Masuala kumi muhimu n ...

Masuala kumi muhimu na mafupi kuhusu mwezi wa Muharram

UJUMBE KWA ALIYEICHOM ...

UJUMBE KWA ALIYEICHOMA KURANI