Nakala

Umilele wa Akhera


Starehe za dunia ni za kupita wakati furaha ya akhera ni ya kudumu na ya milele. Katika maisha haya mtu anapofurahia kitu, ni muda mfupi tu kabla ya kuchoshwa nacho na kuendelea kutafuta kitu anachohisi ni bora zaidi, au anaweza asihisi kukihitaji kabisa. Kwa starehe za Peponi, kamwe mtu hatahisi kuchoshwa na kitu chochote, bali wema wake utaongezeka kila wanapojishughulisha humo.





Pia maisha ya dunia hii ni mafupi sana. Wanadamu wanaishi hapa duniani kwa muda mfupi tu, na ni watu wachache sana wanaofikia umri wa miaka sabini.





“…Sema: Starehe ya dunia ni ndogo, na Akhera ni bora zaidi kwa mwenye kuchamngu...” (Kurani 4:77)





Kuhusu Peponi, watu wataishi milele. Mungu anasema:





“...matunda yake ni ya daima, na pia kivuli chake…” (Kurani 13:35)





“Mlivyo navyo vitakwisha na vilivyoko kwa Mwenyezi Mungu ndivyo vitakavyo bakia …” (Kurani 16:96)





“Hakika hii ndiyo riziki yetu isiyo malizika.” (Kurani 38:54)





Furaha ya Juu


Furaha za watu wa Peponi, kama vile mavazi, chakula, vinywaji, mapambo na majumba yao, zitakuwa bora zaidi kuliko wenzao wa dunia hii. Kwa hakika hakuna nafasi ya kulinganisha, kwani hata nafasi ndogo kabisa katika Pepo ni bora kuliko dunia hii na vyote vilivyomo ndani yake. Mtume Muhammad, rehema na amani ziwe juu yake, amesema:





“Nafasi ya upinde ya mmoja wenu katika Pepo ni bora kuliko zote ambazo jua uchomoza” (Mishkaat al-Masaabiyh 3/85, na. 5615).





Hakuna Uchafu wowote


Pepo haina uchafu wowote wa ulimwengu huu. Kula na kunywa katika maisha haya husababisha haja ya kutoa kinyesi na harufu zake mbaya. Ikiwa mtu anakunywa divai katika ulimwengu huu, anapoteza akili. Wanawake katika ulimwengu huu hupata hedhi na kuzaa, ambayo ni vyanzo vya maumivu na uchungu. Pepo haina usumbufu huu wote: watu wake hawatakojoa, kujisaidia, kutema mate au kuteseka na ugonjwa wa mafua. Mvinyo wa Peponi, kama ilivyoelezwa na Muumba wake, ni:





“Kinywaji cheupe, kitamu kwa wanywao, Hakina madhara, wala hakiwaleweshi.” (Kurani 37:46-47)





Maji ya Peponi hayana chumvi, na ladha ya maziwa yake haibadiliki:





“...mito ya maji yasiyo vunda, na mito ya maziwa isiyo haribika ladha yake...” (Kurani 47:15)





Wanawake wa Peponi ni wasafi na hawana hedhi, kutokwa na damu baada ya kuzaa na uchafu mwingine wote unaowapata wanawake katika dunia hii, na wote hawatakua na kinyesi. Mungu anasema:





“...na humo watakuwa na wake walio takasika…” (Kurani 2:25)





Mtume alimjibu mtu pale walipomuuliza vipi watu wa Peponi watajisaidia:





"Wanajisaidia kwa kutokwa na jasho kwenye ngozi zao, na harufu yake itakuwa ya miski, na matumbo yote yatakua yamekonda." (ibn Hibbaan)





Hayo tuliyoyataja yamekuwa ni ulinganisho tu ili kuelewa asili ya Pepo, lakini kama Mungu alivyosema, furaha yake imefichwa kweli.





“Nafsi yoyote haijui waliyo fichiwa katika hayo yanayo furahisha macho - ni malipo ya yale waliyo kuwa wakiyatenda.” (Kurani 32:17)





Peponi: Hakuna Kitu Mfano Wake


Furaha za Peponi zinazidi mawazo na kupitiliza maelezo. Hakuna mfano wake kwenye vitu vinavotambulika na watu kwenye ulimwengu huu; hata tuwe na maendeleo kiasi gani, tunachopata sio kitu kwa kulinganisha na furaha ya Akhera. Kama ilivyotajwa katika ripoti kadhaa, hakuna kitu kama Pepo:





"Ni mwanga unaometa, mimea yenye kunukia, jumba la kifalme, mto unaotiririka, matunda yaliyoiva, mke mzuri na mavazi tele, katika makao ya milele yenye furaha tele, katika nyumba nzuri za juu zilizojengwa kwa sauti". (Ibn Maajah, Ibn Hibbaan)





Sahabah alimuuliza Mtume kuhusu majengo ya Peponi naye akajibu kwa maelezo ya ajabu:





“Matofali ya dhahabu na fedha, na chokaa ya miski yenye harufu nzuri, kokoto za lulu na yakuti, na udongo wa zafarani. Yeyote anayeingia humo amejawa na furaha na hatahisi huzuni kamwe; ataishi huko milele na hatakufa kamwe; nguo zao hazitachakaa na ujana wao hautanyauka.” (Ahmad, at-Tirmidhi, ad-Daarimee)





Mungu anasema:





“Na utakapo yaona, utakuwa umeona neema na ufalme mkubwa.” (Kurani 76:20)





Kile ambacho Mungu ametufichia furaha ya Peponi ni zaidi ya uwezo wetu wa kufahamu. Mtume alisema kuwa Mwenyezi Mungu alisema:





“Nimewaandalia waja Wangu yale ambayo jicho halijaona, sikio halijasikia na moyo wa mwanadamu hauwezi kufikiria.” Soma kama unataka:





“Nafsi yoyote haijui waliyo fichiwa katika hayo yanayo furahisha macho - ni malipo ya yale waliyo kuwa wakiyatenda.” (Kuran 32:17)





Katika ripoti nyingine:





“Usijali Mungu amekuambia nini; yale ambayo Yeye hajakuambia ni makubwa zaidi.” (Saheeh Muslim)





Katika makala nyingine, tutajaribu kutaja baadhi ya maelezo makhsusi ya Pepo na starehe zake zilizoelezwa kwetu na Mwenyezi Mungu na Mtume Wake wa mwisho.



Machapisho ya hivi karibuni

UJUMBE KUTOKA KWA MUH ...

UJUMBE KUTOKA KWA MUHUBIRI MUISLAMU KWA MKRISTO

FADHILA YA KUFUNGA SI ...

FADHILA YA KUFUNGA SIKU SITA ZA SHAWAL

Masuala kumi muhimu n ...

Masuala kumi muhimu na mafupi kuhusu mwezi wa Muharram

UJUMBE KWA ALIYEICHOM ...

UJUMBE KWA ALIYEICHOMA KURANI