Artikler

Ushuhuda


Awali, makafiri wa Makka walisema Muhammad ndiye mwandishi wa Kurani. Mwenyezi Mungu akawajibu:





"Au ndio wanasema: Ameitunga hii! Bali basi tu hawaamini! Basi nawalete masimulizi kama haya ikiwa wao wanasema kweli. Au wao wameumbwa pasipo kutokana na kitu chochote, au ni wao ndio waumbaji?" (Kurani 52:33-35)





Kwanza, Mungu aliwapa wito walete sura kumi zinazofanana na Kurani:





"Au wanasema: Ameizua? Sema: Basi leteni Sura kumi zilizo zuliwa mfano wa hii, na waiteni muwawezao badala ya Mwenyezi Mungu, ikiwa mnasema kweli. Na wasipo kuitikieni, basi jueni ya kwamba (hii Kurani) imeteremshwa kwa ujuzi wa Mwenyezi Mungu, na kwamba hapana Mungu ila Yeye. Basi je! Nyinyi ni Waislamu?" (Kurani 11:13-14)





Lakini, waliposhindwa kuleta sura kumi, Mungu aliipunguza hadi sura moja:





"Na ikiwa mna shaka kwa hayo tuliyo mteremshia mja wetu basi leteni sura moja ya mfano wake, na muwaite mashahidi wenu badala ya Mwenyezi Mungu, ikiwa mnasema kweli. Na mkitofanya - na wala hamtofanya kamwe - basi uogopeni moto ambao kuni zake ni watu na mawe walio andaliwa hao wanao kanusha."(Kurani 2:23-24)





Hatimaye, Mungu alitabiri kushindwa kwao milele kuitikia wito huo wa Mungu:





"Sema: Wangeli kusanyika watu na majini [1] ili walete mfano wa hii Kurani basi hawaleti mfano wake, hata wakisaidiana wao kwa wao!’" (Kurani 17:88)





Mtume wa Uislamu anasema:





"Kila Nabii alipewa ishara ili watu wamwamini . Hakika mimi nimepewa Ufunuo wa Mwenyezi Mungu ambao Mwenyezi Mungu amenifunulia. Kwa hiyo natumai kuwa nitakuwa na wafuasi wengi kati ya manabii wote siku ya Kiyama." (Saheeh Al-Bukhari)





Miujiza iliyofanywa na manabii ilikuwa ya wakati maalum, na kuwalenga tu wale walioishuhudia, ilhali mfano wa muujiza wa Mtume wetu, Kurani Tukufu, haukupewa nabii mwingine yeyote. Ubora wake wa lugha, mtindo, uwazi wa ujumbe, nguvu za hoja zake, ubora wa maswali yake, na kushindwa kwa wanadamu kuleta mfano wa hata sura yake fupi hadi mwisho wa dunia ni miujiza ya kipekee. Wale ambao walishuhudia ufunuo na wale waliofuata, wote wanaweza kunywa kutoka kwa chemchemi yake ya hekima. Ndiyo sababu Nabii wa Rehema alitumai kuwa atakuwa na wafuasi wengi kati ya manabii wote, na kutabiri haya kwa wakati ambapo Waislamu walikuwa wachache mno, lakini baada ya hapo watu wakaanza kukubali Uislamu kwa wingi. Hivyo, utabiri ulikuja kutimia.





Kwa nini Mfano wa Kurani Hauwezi Kuletwa


Hali ya Mtume Muhammad


Alikuwa mwanadamu wa kawaida.





Hakuwa na uwezo wa kuandika wala kusoma.





Alikuwa na umri zaidi ya miaka arubaini alipopata ufunuo wa kwanza. Kabla ya hapo hakuwa mlumbi au malenga, alikuwa mfanya biashara tu. Hajawahi kutunga shairi hata moja au kutoa hutuba hata moja kabla ya kuchaguliwa kuwa nabii.





Alileta kitabu na kusema kimetoka kwa Mungu, na Waarabu wote wa wakati wake walikubaliana kuwa hakuna aliyeweza kuleta mfano wake. 





Wito wa Kurani


Kurani inampa changamoto yeyote anayempinga Nabii. Changamoto ni kuleta sura (surah) inayofanana nayo, hata kama ni kutokana na juhudi za pamoja. Mtu anaweza kutafuta msaada wowote anaoweza kupata kutoka kwa ulimwengu wa kimwili na wa kiroho.





Mbona Wito huu?


Kwanza, Waarabu walikuwa washairi. Mashairi yalikuwa pambo lao kuu na aina yao ya uwakilishi. Ushairi wa Kiarabu ulitegemea mdomo kwa kiasi kikubwa ; ulikuwa sauti kabla ya kupata herufi. Washairi wangeweza kutunga mashairi mazuri hapo hapo na kuhifadhi akilini maelfu ya mishororo. Waarabu walikuwa na mfumo mgumu wa kutathmini mshairi na mashairi yalitakikana kufikia viwango vigumu. Mashindano ya kila mwaka yalichagua 'sanamu' za mashairi, na yalichorwa kwa dhahabu na kuwekwa ndani ya Kaaba, pamoja na sanamu zao za ibada. Wenye ujuzi zaidi ndio waliokuwa majaji. Washairi wangeweza kuleta vita au amani kati ya makabila yanayopigana. Walielezea wanawake, mvinyo, na vita kushinda watu wengine wote.





Pili, wapinzani wa Mtume Muhammad walikuwa na azimio kubwa la kukomesha utume wake kwa njia yoyote iwezekanavyo. Mungu aliwapa njia isiyo ya vurugu ya kumpinga Muhammad.





Kutoweza Kuitikia Wito na Matokeo yake


Historia ni shahidi kwamba Waarabu wa kabla ya Uislamu hawakuweza kuleta hata sura moja ili kuitikia wito wa Kurani.[2] Badala yake, walichagua vurugu na kupigana vita dhidi yake. Wao, kati ya watu wote, walikuwa na uwezo na nia ya kushinda changamoto ya Kurani, lakini hawakuweza kufanya hivyo. Na lau kuwa wangeli fanya hivyo basi wangeli thibitisha uongo wa Kurani, Na yule aliye ileta Kurani hiyo bila ya shaka angeli dhihirishwa kuwa ni Mwongo. Ukweli kwamba Waarabu wa kale hawakuweza kutimiza changamoto hii ni ushahidi tosha kuwa Kurani haiwezi kufananishwa. Mfano wao ni wa mtu mwenye kiu karibu na kisima. Sababu pekee ya kufa kwa kiu ni kama hakuweza kufika maji!





Zaidi ya hayo, kutokuwa na uwezo kwa Waarabu waliopita kuitikia wito wa Kurani kunamaanisha kuwa Waarabu wa baadaye hawana uwezo wa kuitikia, kutokana na ukosefu wao wa ustadi wa Kiarabu wa kitambo waliokuwa nao Waarabu waliotangulia. Kwa mujibu wa wataalamu wa lugha ya Kiarabu, Waarabu kabla na wakati wa Mtume, bila kuongeza vizazi vilivyofuata, walikuwa na ustadi kamili wa lugha ya Kiarabu, sheria zake, na mashairi yake. Waarabu waliowafuata hawakuwa na ustadi wa Waarabu wa Kale.[3]





Mwishowe, changamoto ni kwa Waarabu na wasio Waarabu pia. Iwapo Waarabu hawawezi kutoa mfano wa Kurani, wasio zungumza kwa Kiarabu hawawezi kudai kuwa wanaweza. Kwa hivyo, kutokuwa na uwezo wa kutoa mfano wa Kurani ni changamoto kwa wasio Waarabu pia.





Itakuwaje kama mtu angesema: ‘pengine changamoto ya Kurani ilikabiliwa na mtu fulani katika zama za Mtume, lakini kurasa za historia hazikuhifadhi.’?


Tangu mwanzo, watu wameripoti matukio muhimu kwa vizazi vyao vilivyowafuata, hasa katika yale yanayostaajabisha au yale watu wanayasubiri. Wito wa Kurani ulikuwa umeenea vizuri na ulijulikana, na kama mtu aliutimiza, ingekuwa haiwezekani kwa jambo hilo kutotufikia. Ikiwa imepotea katika kumbukumbu za historia, basi, inawezekana pia kwamba kulikuwa na zaidi ya Musa mmoja, zaidi ya Yesu mmoja, na zaidi ya Muhammad mmoja; labda maandiko mengi pia yalifunuliwa kwa manabii hawa wasiojulikana, na inawezekana ulimwengu haujui chochote kuhusu hilo! Kama vile fikra hizi hazina msingi wa kihistoria, pia si hekima kufikiria kuwa wito wa Kurani uliitikiwa bila ya sisi kujua.[4]





Pili, lau wangeitikia wito huo, Waarabu wangemkataa Nabii. Ingekuwa chombo chao kikubwa cha kumdhihaki na kumpinga. Hakuna kitu kama hiki kilichotokea, badala yake, walichagua vita.





Ukweli kwamba hakuna juhudi za wasio Waislamu zimefanikiwa katika 'kutoa aya' kama aya za Kurani inamaanisha kuwa hakuna mtu aliyejali Kurani sana mpaka akafanya juhudi, au kwamba walifanya juhudi, lakini hawakufanikiwa. Hii inaonyesha kuwa Kurani haina mfano, ni ujumbe wa kipekee na wa milele. Upekee wa Kurani pamoja na ujumbe wa Mungu unaoletea wanadamu ni dalili ya uhakika ya ukweli wa Uislamu. Baada ya kujua hilo, kila mtu anakabiliwa na moja kati ya mawili. Akubali kwa uwazi kuwa Kurani ni Neno la Mungu. Kwa kufanya hivyo lazima akubali pia kwamba Muhammad alitumwa na Mungu na alikuwa Mtume wake. Au anajua kwa siri kuwa Kurani ni kweli, lakini anachagua moyoni mwake kuikataa. Ikiwa mtu huyo ni mwaminifu katika kutafuta kwake, anahitaji tu kuchunguza swala hili la Kurani kutokuwa na kifani ili kulea uhakika wake wa ndani kwamba amepata ukweli wa mwisho katika dini ambayo inatumia Kurani.



Nye innlegg

DYD AV Å FASTE SKS DA ...

DYD AV Å FASTE SKS DAGER MED SHAVAL

Førti hadither av Ima ...

Førti hadither av Imam Nawawi

SPØRSMÅL OM SEX OG IN ...

SPØRSMÅL OM SEX OG INTIMITETSPROBLEMER FIKK SVAR 1 (ISLAMSK UTSIKT)

30 TIPS FOR Å FORBERE ...

30 TIPS FOR Å FORBEREDE DEG TIL RAMADAN I SHABAN